MGENI KWETU NYUMBANI
Unashangaa nini?
Msiba kwetu nyumbani
Kisiwani mwa amani
Kizazi hadi kizazi
Sisi tumeuzoea…
Mgeni kwetu nyumbani
Kamwe si hayawani
Twamthamini mgeni
Kuliko hata mwenyeji
Sisi tunampokea…
Biashara kwetu ndani
Haikosi mshitiri
Bara hata visiwani
Nyanda juu hadi pwani
Sisi tunaiwezesha…
Walokuja kwa jahazi
Wakisukumwa na kusi
Wa merikebu za mbali
Mizinga zikisheheni
Sisi tuliwaitika…
Wengine wakichuuza
Na baadhi kulowea
Bara wakitangatanga
Kuzitafuta ngawira
Sisi tuliwaonyesha…
Nasi hatukukaidi
Kuwapokea kwa jadi
Walipoibisha hodi
Na misafara kuhodhi
Sisi tuliwapenyeza…
Hatukuuanza leo
Ukuwadi tufanyao
Tulianzia na hongo
Kwa kila jino la tembo
Sisi tulijitwalia…
Mambo yalipogeuka
Tukageuzwa ngawira
Ndiposa wenye dhamana
Bei walipotupiga
Sisi tuliwahofia…
Ni hawa hawa wakuu
Wa jana na leo yetu
Wanaofanya mizungu
Kutugeuza vizuu
Sisi tunawatazama…
Wametuweka jamvini
Kututia msibani
Tulie kwa ufakiri
Na mali zetu lukuki
Sisi tumehamanika…
Leo ushangae nini
Kwani ulikuwa wapi
Nyuki wakipigwa moshi
Na kulala usingizi
Sisi tukisuasua…
Masega yalipovunjwa
Na asali ikarinwa
Na wanapozindukana
Nta wakasake tena
Sisi tulinung’unika…
Lini tutakuwa mbogo
Tuyakatae makombo
Tukashikane mikono
Tusitoe shikamoo?
Sisi tunajiuliza!
©demere kitunga, 2012
0 comments:
Post a Comment